Esther Matiko aweka wazi kiu yake ya kuwa Spika wa Bunge
Mbunge wa Tarime Mjini , Esther Matiko (CHADEMA) amebainisha kwamba endapo atapata nafasi ya kuwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, chama chake itabidi kimsamehe kwa kuwa atasimamia kanuni zote na sheria bila kupendelea chama.
Matiko amedai kwa upande wake angeliacha bunge lifanye kazi ya kuisimamia serikali, kuishauri pamoja na kutunga sheria bila kupendelea chama chochote.
Matiko amesema kuwa anakiombea sana Chama chake kiweze kushika dola ili 2020 aweze kugombea nafasi ya uspika wa bunge kabla hajaianza safari ya urais kwa miaka inayokuja.
"Mwaka 2020 nadhani nitagombea nafasi hiyo ya Spika nakiombea chama changu kishinde na kuongoza serikali. Nikiwa Spika nitasimamia misingi na utaratibu pamoja na kusimamia nini kazi ya bunge. Kazi ya bunge mojawapo ni kusimamia na kuishauri serikali hivyo kama ni mbunge wa chama changu au hata wa upinzani akisimama kuisimamia vyema na kuishauri serikali ningemuacha aongee, ndiyo kazi ya bunge na hiyo ndiyo njia ya kuishauri serikali pale ambapo inaenda kinyume na mambo yanayotarajiwa," Matiko.
Matiko ameongeza "Ningekuwa nawaambia ukweli kabisa hata kwenye vikao vya chama kwamba mimi ni spika na bunge ni muhimili unaojitegemea katika kutunga sheria na serikali ni muhimili mwingine hivyo chama changu itabidi kinisamehe kwa hilo. Ningekuwa spika wa mfano. Ningewashauri kwamba ikipitishwa bajeti wakaitekeleze siyo bunge linapitisha bajeti hii serikali inatekeleza vingine wakati mimi ni spika".
No comments